Mark 13:3-23

Mateso Yatabiriwa

(Mathayo 24:3-14; Luka 21:7-19)

3 aYesu alipokuwa ameketi kwenye Mlima wa Mizeituni mkabala na Hekalu, Petro, Yakobo, Yohana na Andrea wakamuuliza faraghani, 4 b“Tafadhali tuambie, mambo haya yatatukia lini? Nayo dalili ya kuwa hayo yote yanakaribia kutimia itakuwa gani?”

5 cYesu akawaambia: “Jihadharini mtu yeyote asiwadanganye. 6Wengi watakuja kwa Jina langu wakidai, ‘Mimi ndiye,’ nao watawadanganya wengi. 7Msikiapo habari za vita na uvumi wa vita, msiwe na hofu. Mambo haya hayana budi kutukia, lakini ule mwisho bado. 8 dTaifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme. Kutakuwa na mitetemeko sehemu mbalimbali na njaa. Haya yatakuwa ndio mwanzo wa utungu.

9 e “Lakini ninyi jihadharini. Kwa maana watawapeleka katika mabaraza yao na kupigwa mijeledi katika masinagogi. Mtashtakiwa mbele ya watawala na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushuhuda kwao. 10 fNayo habari njema lazima ihubiriwe kwanza kwa mataifa yote kabla ule mwisho haujawadia. 11 gMtakapokamatwa na kushtakiwa, msisumbuke awali kuhusu mtakalosema. Semeni tu lolote mtakalopewa wakati huo, kwa kuwa si ninyi mtakaokuwa mkinena, bali ni Roho Mtakatifu.

12 h “Ndugu atamsaliti ndugu yake ili auawe, naye baba atamsaliti mtoto wake. Watoto nao wataasi dhidi ya wazazi wao na kusababisha wauawe. 13 iWatu wote watawachukia kwa ajili ya Jina langu. Lakini yule atakayevumilia hadi mwisho ataokolewa.

Chukizo La Uharibifu

(Mathayo 24:15-28; Luka 21:20-24)

14 j “Mtakapoona ‘chukizo la uharibifu’ limesimama mahali pasipolipasa (asomaye na afahamu), basi wale walioko Uyahudi wakimbilie milimani. 15Yeyote aliye juu ya dari ya nyumba asishuke au kuingia ndani ili kuchukua chochote. 16Aliye shambani asirudi nyumbani kuchukua vazi lake. 17 kOle wao wenye mimba na wale wanaonyonyesha watoto siku hizo! 18Ombeni mambo haya yasitokee wakati wa baridi. 19 lKwa maana siku hizo zitakuwa za dhiki kuu ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo, hapo Mungu alipoumba ulimwengu, mpaka leo, na wala haitakuwako tena kamwe. 20Kama Bwana asingelifupisha siku hizo, kamwe asingeliokoka mtu yeyote. Lakini kwa ajili ya wateule, wale aliowachagua, amezifupisha siku hizo. 21 mWakati huo mtu yeyote akiwaambia, ‘Tazama, Kristo
Kristo maana yake ni Masiya, yaani Aliyetiwa mafuta.
huyu hapa!’ au, ‘Tazama, yuko kule,’ msisadiki.
22 oKwa maana watatokea makristo wa uongo na manabii wa uongo, nao watafanya ishara na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale wateule. 23 pHivyo jihadharini. Nimekwisha kuwaambia mambo haya yote mapema kabla hayajatukia.

Copyright information for SwhNEN